Jumamosi, Novemba 29, 2014

SERIKALI imesimamisha leseni ya kampuni ya matatu ya Nazigi Sacco kwa muda wa wiki mbili, baada ya wahudumu wake kushtakiwa kwa kumvua mwanamke nguo katika Barabara ya Thika.

Mkurugenzi wa Mamlaka ya Kitaifa ya Uchukuzi (NTSA) Francis Meja aliipa  kampuni hiyo wiki mbili kuwasilisha magari yao yote 243 kwa ukaguzi. Sacco hiyo ina magari takriban 243.

Kamanda wa Trafiki Charlton Mureithi pia atahakikisha kuwa hakuna gari lolote la kampuni hiyo ambalo litahudumu hadi suala hilo litatuliwe.

 Bw Nicholas Chege Mwangi, dereva wa basi nambari KBT 903R la Githurai 44, akiwa kortini Novemba 28, 2014.

Serikali pia inachunguza matatu ambazo zilihusika katika visa vingine viwili katika majuma mawili yaliyopita katika eneo la Kayole na barabara ya Tom Mboya.

Dereva na makanga wa basi moja la sacco hiyo ambapo abiria mmoja mwanamke alivuliwa nguo na kudhulumiwa kimapenzi kwa saa kadha wataendelea kuzuiliwa kwa siku 21 zijazo, huku polisi wakiendelea na uchunguzi wao.

Bw Nicholas Chege Mwangi na Bw Meshack Mburu Mwangi, ambao ni dereva na utingo wa basi hilo, lenye nambari za usajili KBT 903R wanazuiliwa katika kituo cha polisi cha Kasarani na wanatarajiwa kuwafichua wahusika, ambao wanasemekana kutoroka.

Mahakama Nairobi iliambiwa kuwa polisi walikuwa wakichunguza visa mbalimbali vya dhuluma za kimapenzi, na wameanzisha uchunguzi dhidi ya visa kadha vya dhuluma za kimapenzi na kuvuliwa nguo kwa wanawake jijini Nairobi, ili kuwakamata na kuwashtaki wahusika.

Upande wa mashtaka pia uliwaomba waathiriwa wa dhuluma hizo, ambao hawajajitokeza baada ya kushambuliwa katika maeneo hayo mawili kujitokeza ili kuandikisha taarifa kwani washukiwa hao tayari washakamatwa.

Kuzua hofu

“Kumekuwa na ongezeko la kuvuliwa nguo kwa wanawake pamoja na dhuluma za kimapenzi, hali ambayo imezua hofu miongoni mwa umma. Uchunguzi tuliofanya ulipelekea kukamatwa kwa washukiuwa mnamo Novemba 27 katika Barabara ya Thika,” akasema Duncan Ondimu, ambaye ni kiongozi wa mashtaka katika wasilisho lake kwa mahakama.

Katika kesi tofauti, polisi mmoja wa utawala na abiria mmoja wa kiume wamefikishwa mahakamani kwa kujaribu kumvua nguo msichana mmoja, aliye mwanafunzi mmoja wa shule katika basi moja.

Watu watano pia wameshtakiwa kwa kuwatoa wanawake nguo katika mtaa wa Kayole. Kisa hicho, ambacho kilifanyika katika mtaa wa Kayole kingali kinachunguzwa. Tukio la barabara ya Tom Mboya pia lingali kinachunguzwa.

Jana, upande wa mashtaka ulisema kuwa waliwahoji washukiwa hao wawili lakini “hawakuwa bado wamewafichua washukiwa waliohusika katika kitendo hicho” lakini walikuwa wakifuata habari muhimu zitakazopelekea kukamatwa kwao.

Kiongozi huyo wa mashtaka alisema kuwa mhusika katika kisa cha basi la Githurai 44 bado hajatambuliwa.


0 comments:

Chapisha Maoni