Alhamisi, Januari 23, 2014

Watoto 160,000 huzaliwa wakiwa na maambukizi ya virusi vya ukimwi (VVU) kila mwaka duniani.

Hayo yalisemwa jana jijini Dar es Salaam kwenye uzinduzi wa mpango wa tiba mpya ya dozi ya kidonge chenye mchanganyiko wa dawa aina tatu maarufu kama PMTCT Option B+, unaolenga kupunguza kiwango cha maambukizi ya VVU kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto wakati wa kujifungua.

Mpango huo unamtaka mama mjamzito kunywa kidonge kimoja cha ARV chenye mchanganyiko wa dawa aina tatu kwa maisha yake yote kabla na baada ya kujifungua, tofauti na ule wa kwanza uliojulikana kwa jina la A+ ambao mama alitakiwa kunywa vidonge vya ARV kabla ya kujifungua na baada ya kujifungua huacha dozi.

Akizindua mpango huo, mke wa Rais ambaye pia ni Mwenyekiti wa Taasisi ya Maendeleo na Wanawake (Wama), Salma Kikwete, alisema Tanzania ni miongoni mwa nchi 20 duniani zenye maambukizi makubwa ya VVU na kwamba takribani watoto 160, 000 huzaliwa wakiwa na maambukizi ya virusi hivyo.

Alisema kati ya idadi hiyo, watoto 128,000 huzaliwa na VVU kwa kuambukizwa kutoka kwa mama zao wakati wa kujifungua na 32,000 huambukizwa virusi hivyo kwa njia nyingine, na wote hufariki wakiwa chini ya umri wa miaka mitano.

Mama Salma Kikwete aliongeza kuwa, mpango huo ambao umeridhiwa na serikali, unalenga kupunguza kiwango cha maambukizi kwa watoto wakati kutoka kwa mama zao ambao wanaishi na VVU wakati wa kujifungua.

Kwa mujibu wa Salma Kikwete, mpango huo utamwezesha mama anayeishi na VVU kuendelea na uzazi kama kawaida huku akizaa watoto ambao hawana maambukizi yoyote ya virusi hivyo.

0 comments:

Chapisha Maoni